Monday, January 14, 2013

TAMASHA LA WASANII KUFANYIKA DAR LIVE JANUARI 26

 
Mwakilishi kutoka kampuni ya Vannedrick Tanzania Ltd, ambao ni moja ya waandaaji wa tamasha hilo, Dino Debwe, akiongea na wanahabari (hawapo pichani).
 
Rais wa Shirikisho la Filamu Tanzania (TAFF), Simon Mwakifwamba, naye akiongea machache wakati wa mkutano huo na wanahabari.
 
Baadhi ya wasanii wa filamu nchini kutoka kushoto ni Dk Cheni, Snura, Shamsa Ford na Shilole wakifuatilia mkutano huo.
 
 Sehemu ya wanahabari waliohudhuria mkutano huo uliofanyika katika hoteli ya Lamada Ilala jijini Dar leo.
Kitalima Gerald na Khatimu Naheka
SHIRIKISHO la Filamu Tanzania (TAFF), limeandaa Tamasha la Wasanii litakalofanyika Januari 26, mwaka huu kwenye Ukumbi wa Dar Live uliopo Mbagala Zakhem jijini Dar es Salaam.
Akizungumza na waandishi wa habari leo jijini Dar es Salaam, rais wa shirikisho hilo, Simon Mwakifwamba, alisema tamasha hilo wamelipa jina la Siku ya Ma-Star wa Filamu Tanzania, likiwa na lengo la kupata fedha za kujiendesha.
Mwakifwamba alisema wanakabiliwa na changamoto nyingi ikiwemo kukosa ofisi na vitendea kazi muhimu ndani ya ofisi kulingana na hadhi, hivyo wanakadiria kupata shilingi milioni 60 katika tamasha hilo.
Alisema kwa kutambua hilo wameliandaa tamasha hilo wakiamini kupata wadau wengi wapenzi wa kazi zao.
Kiingilio kwa watoto kitakuwa Sh 2,000, wakubwa 7,000 na VIP 15,000. Tamasha litaanza saa 4:00 asubuhi.
“TAFF tumeandaa Tamasha la Wasanii tulilolipa jina la Siku ya Ma-Star wa Filamu Tanzania, litakalofanyika Januari 26, mwaka huu kwenye Ukumbi wa Dar Live.
“Lengo ni kupata fedha kwa ajili ya kukabiliana na changamoto zinazotukabili, ikiwemo kuwa na ofisi kulingana na hadhi yetu na vitendea kazi muhimu ndani ya ofisi, tumekadiria kupata shilingi milioni 60 katika tamasha hilo linalotarajiwa kuanza saa nne asubuhi,” alisema Mwakifwamba.
by mrisho's blog

No comments:

Post a Comment